RAIS DKT. JOHN POMBE MAGUFULI KAMALIZA ZIARA YA SIKU 4 MIKOA YA LINDI PWANI NA MTWARA.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli jana tarehe 05 Machi, 2017 amemaliza ziara yake ya kikazi ya siku 4 katika mikoa ya Pwani, Lindi na Mtwara.

 



Kabla ya kuondoka Mjini Mtwara na kurejea Jijini Dar es Salaam Mhe. Rais Magufuli alifanya mkutano wa hadhara katika Uwanja wa Mashujaa Mjini Mtwara ambapo alisema Serikali ya Awamu ya Tano imejipanga kuhakikisha inasukuma maendeleo ya Mtwara na Lindi kwa nguvu kubwa kwa manufaa ya wananchi.

Alisema Serikali imedhamiria kutilia mkazo juhudi za uendelezaji wa bandari ya Mtwara, ujenzi wa barabara, uimarishaji wa miundombinu ya nishati ya umeme, ujenzi wa viwanda vikubwa na usimamizi mzuri wa shughuli za kilimo ambavyo vitasaidia kukuza uchumi, kuzalisha ajira na kuboresha maisha ya watu.

Mhe. Rais Magufuli aliwapongeza viongozi na wananchi wa Mkoa wa Mtwara kwa mafanikio yaliyopatikana katika soko la korosho lililopita na ameagiza wale wote waliohusika kufuja fedha za wakulima wachukuliwe hatua.

Aidha, Mhe. Dkt. Magufuli alisema Tanzania itaendeleza uhusiano na ushirikiano wake mzuri na nchi jirani ya Msumbiji na ametaka suala la wahamiaji haramu wanaoondolewa nchini humo wakiwemo Watanzania lisikuzwe huku akisisitiza kuwa Serikali haiwezi kuwatetea watu wanaoishi katika nchi nyingine bila kufuata sheria.

Kuhusu Mkoa wa Mtwara kufanya vibaya kielimu, Mhe. Rais Magufuli amewataka wananchi wa Mtwara kubadilika kwani juhudi za Serikali kuwapelekea maendeleo hazitakuwa na maana kama wananchi watakuwa hawana elimu.

“Nimeambiwa hapa watu wanapenda sana disco na ngoma, watoto badala ya kusoma wanacheza disco, hapo tunakwenda pabaya” alisisitiza Mhe. Rais Magufuli.

Mkutano wa Mhe. Rais Magufuli Mjini Mtwara ulidhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi, Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Muhongo, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa, Waziri wa Fedha na Mipango Dr. Philip Mpango, Wabunge na viongozi wa taasisi.


Xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx


Hatimaye gazeti la MAWIO lililofutwa na serikali ya Tanzania na kuacha kuchapishwa kwa zaidi ya mwaka mmoja, limerejea mtaani kwa uamuzi wa Mahakama Kuu.

Serikali ililifuta gazeti hilo na kulizuia kuchapishwa kwa njia yoyote ile Januari 15, mwaka jana- 2016.

Uamuzi wa Mahakama Kuu uliotolewa Jumanne , umetupilia mbali amri ya serikali ya “kuliua na kulizika kabisa” gazeti hilo lililokuwa likitoka kila wiki – Siku ya Alhamisi.

Mahakaka Kuu ilisema kuwa amri ya serikali kuliua MAWIO haikuwa sahihi, hivyo “gazeti hilo lilionewa.”

Jopo la majaji watatu, likiongozwa na Jaji Sakieti Kihiyo, limesema gazeti la MAWIO halikupewa nafasi ya kujitetea kabla ya hatua ya serikali ya kulifuta kutoka orodha ya msajili wa magazeti nchini.

Msajili wa magazeti nchini ni Idara ya Habari Tanzania (MAELEZO).

Jaji Ignas Kitusi ndiye alisoma uamuzi wa Mahakama kuu – kwa niaba ya jopo siku ya Jumanne, wiki iliyopita (Februari 28). Jaji mwingine aliyekuwa kwenye jopo hilo, ni Jaji Ama-Isario Munisi.

Serikali ililifuta gazeti la MAWIO tarehe 15 Januari 2016 baada ya kudaiwa kuandika ilichoita habari na makala za “kichochezi.”

Utawala wa Kampuni ya Victoria Media Services Limited, wachapishaji wa gazeti la MAWIO, uliamua kufungua kesi mahakamani. Hii ni kesi Na. 15 ya mwaka 2016.

Wakili wa MAWIO, Dk. Rugemeleza Nshalla, amesema kuwa hatua ya serikali iliegemea falsafa ya “…Nyonga kwanza na sikiliza baadaye.”

Dk. Nshalla amesema katika mazingira yoyote yale, sharti walalamikiwa wapate nafasi ya kujieleza na kusiklilizwa na mahakama kwanza kabla ya hukumu kutolewa.

Mkurugenzi Mtendaji na Mhariri Mkuu wa gazeti la MAWIO, Simon Mkina amesema alishangazwa sana na hatua ya serikali kufuta alichoita “mdomo wa wananchi.”

“Kufuta chombo hiki au kingine kama hiki, ni kukiri kuwa serikali haipendi kusikia kutoka kwa wananchi…” amesema Mkina

Mkina amesema MAWIO limekuwa gazeti linalozingatia maadili na kufuata weledi wa hali ya juu katika kuandika na kuchapisha habari na makala na kuongeza kuwa limekuwa gazeti pekee linalotoa uwanja mpana kwa wananchi kuandika mawazo yao ili kuchochea uwajibikaji wa viongozi wa serikali.

Mkina amesema kufuatia uamuzi huo wa Mahakama Kuu, MAWIO litarejea mtaani Alhamisi ya wiki hii na kuahidi kuwapa wasomaji wake habari zilizofanyiwa kazi ya ziada.

“Kwa muda wa zaidi ya mwaka mmoja, wakati gazeti halipo mtaani – likiwa limefutwa na serikali, pamoja na kupoteza ajira za watu na kuingia katika hasara kubwa, bado tulikuwa na kazi ya kujiuliza ni wapi tulikosea na je, lini tutapewa haki yetu? Bahati nzuri haki yetu imefika,” aliongeza Mkin.

Uamuzi na hatua ya kulifuta MAWIO, lililokuwa likichapishwa kila Alhamisi, ulitangazwa na Nape Nnauye, Waziri wa habari, vijana, utamaduni, sanaa na michezo.

Tangazo lililotolewa katika gazeti la serikali, Na. 55 la Januari 15, 2016, lilisema serikali inachukua uamuzi wa kulifuta kwa mujibu wa mamlaka iliyonayo kupitia Sheria ya Magazeti ya 1976; sura ya 229 kifungu cha 25(1).


Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 maoni:

Post a Comment