GWAJIMA ATOA JIPU AMTAKA DAUD BASHITE AJITOKEZE KUTHIBITISHA VYETI.



Askofu Mkuu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Askofu Josephat Gwajima, amezindua operesheni mpya aliyoipa jina la ‘Operesheni 81Mzizima’ huku akimtaka mtu anayeitwa Daud Bashite ajitokeze hadharani kuthibitisha uhalali wa vyeti vyake.

 

Hivi karibuni, Askofu Gwajima alihubiri kanisani kwake na kusema Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, anatumia vyeti vya mtu anayeitwa Paul Christian, wakati jina lake halisi ni Daud Albert Bashite.

Akizungumza wakati wa ibada kanisani hapo, Ubungo jijini Dar es Salaam jana,  Askofu Gwajima alisema operesheni hiyo mpya ni vita ya mwisho ya kumshikisha mtu adabu.

Alisema, tangu aanzishe hoja hiyo, hadi sasa wahusika hawajajitokeza hadharani kujibu tuhuma hizo, jambo ambalo alisema linaonyesha alichokisema ni kweli.

“Tangu niibue hoja ya Makonda anatumia vyeti vya Daud Albert Bashite, hakuna aliyejitokeza hadharani kukanusha madai yangu.

“Mimi naamini nilisema ukweli kwani kitendo cha kukaa kimya kinaonyesha wazi kuwa ni kweli ninachokisema na kama anabisha, aje hadharani kukanusha akiwa na vyeti vyake na mimi nitakuja na vyangu…

“Kuna baadhi ya watu wananisihi sana niache kumchambua eti wanasema, Gwajima acha, hiyo inatosha.

“Mbona wakati Makonda aliponihusisha na dawa za kulevya hakuna aliyejitokeza kumwambia aache?

“Hii ni vita ya mzizima ya kushikisha adabu iitwayo hold the final battle of good manners,”alisema Askofu Gwajima.

“Hizi ni salamu tu ili ajue kuwa ukimshambulia baba wa imani, hauwezi kubaki salama kwa sababu viongozi wa dini wanapigana vita mbalimbali ikiwamo majini na mashetani, lakini wanashinda kwa jina la Yesu.

“Nina uhakika na nina ushahidi usio na shaka kuhusiana na suala hilo, labda ajitokeze na kuniomba msamaha.

“Nina material na mazagazaga kibao kuhusu Daud Bashite, niseme,” alihoji Gwajima huku waumini wake wakiitikia semaaa.

“Lakini, kwa leo sitaki nimwongelea sana, kwa sababu namwonea huruma, ila ninachotaka kumwambia ni kwamba, usiweke miguu yako kwenye mashine ya kusaga na kukoboa, utageuka sembe.

“Akumbuke kuwa, baba wa familia akiguswa, hata watoto wanaamka, ndicho kilichojitokeza katika maisha yangu kwani baada ya kushambuliwa sana, waumini wameongezeka tofauti na awali.

“Hata wale waliokuwa hawaji kanisani, hivi sasa wanakuja,”alisema. 

Katika mahubiri hayo, Askofu Gwajima alisema kuna wakati Mungu huwainua watu wake kwa makusudi maalumu ili kutimiza kusudio lake.

“Sasa nataka kumwambia kuwa, hizi ni salamu tu, nimerusha ka kipande tu… kuhusu Bashite, lakini kelele kibao.

“Hapa sitaki maigizo wala ngonjera, ninachotaka ni samahani tu, lakini anapaswa kujua kuwa, ukimshambulia baba wa imani, awe askofu, mchungaji, padri au wa dini yoyote, hauwezi kubaki salama, lazima na wewe utashambuliwa tu,”alisema.

Pamoja na hayo, alisema kama ataamua kukaa kimya kama anavyoombwa na baadhi ya watu, akikaa kimya Mungu atawainua watu wengine ili waweze kuzungumza kwa niaba yake.

Kwa mujibu wa Gwajima, hana nia ya kumchafua mtu kwenye suala hilo wala hana mgogoro na hana tatizo, ila aliamua kusema alichokisema kwa sababu alichokozwa.

Pia, Askofu Gwajima alisema ana historia ndefu inayoanzia Oktoba 21, mwaka 1996 wakati alipoanzisha kanisa lake na kupitia changamoto mbalimbali ambazo alizishinda kwa nguvu za Mungu.

Alisema kwamba, hadi sasa ana makanisa 400 yaliyopo maeneo mbalimbali ndhini na mengine 300 yaliyopo katika nchi mbalimbali duniani.

Katika mabuhiri hayo, Askofu Gwajima alimtolea mfano Erick Shigongo kwa kile alichosema kuwa ni miongoni mwa watu wa kuigwa kwani wanatafuta mafanikio kadri wawezavyo.


Wiki iliyopita Jeshi la Polisi kwa mara nyingine lilizingira nyumba ya Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima, kwa kile lilichodai kuwa lilifika kufanya uangalizi.


Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 maoni:

Post a Comment