SAMUEL SITTA AGEUKA MBOGO KWA WANAOMBEZA KWAMBA HAFAI KUWA RAIS WA TZ


sitta
MWENYEKITI wa Bunge Maalum la Katiba, Samuel Sitta, amewashukia wanasiasa wanaomkejeli kwa kudai kuwa hafai kuwa rais na amesisitiza kwamba wenye maamuzi juu ya suala hilo ni wananchi na si vinginevyo.
 

Sitta alitoa kauli hiyo jana bungeni mjini Dodoma wakati akitoa taarifa juu ya utaratibu wa kupokea mawasilisho ya kazi zilizofanywa na Kamati za Bunge Maalum la Katiba.

 

Alisema wapo watu wanaomkejeli na kusema kuwa shughuli ya kuongoza Bunge hilo zimemshinda, hivyo hafai kuwa rais.

 

 Alisema yeye hajaomba urais bali anafanya kazi yake kama Mwenyekiti wa Bunge maalum la Katiba na si vinginevyo.

 

“Nafanya kazi hii kama Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba; haya mengine ya rafiki yangu Juma Haji Duni (Makamu Mwenyekiti wa CUF) eti anajaribu kunipima kwa hoja zilizo duni kabisa,lakini mimi nasema wanaochagua rais ni wananchi,” alisema Sitta na kuongeza;

 

“Inawezekana mwakani wananchi wa Tanzania wakatamani mtu mzima aliyetulia asiyeogopa wapuuzi,wakatamani mtu makini, mwadilifu basi kama itakuwa hivyo, wajue tupo na sisi wengine wa kuweza kufikiriwa kwa mambo kama hayo,” alisema Sitta.

 

Aliwashukia watu wanaokejeli Bunge hilo kwa madai kuwa uwepo wa wajumbe wa Bunge hilo ni kinyume na utaratibu na kusema kuwa wananchi mbalimbali wamebaini kasoro zilizopo katika rasimu kama wajumbe wa Bunge hilo walivyoyaona katika kamati zao wakati wakijadili rasimu hiyo.

 

Alisema kasoro zilizojitokeza katika rasimu hiyo si jambo la ajabu, wala kupuuza kazi iliyofanywa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, kwani ilifanya kazi yake vizuri.

 

“Tukumbuke Tume ilipokea maoni kutoka kwa wananchi na mabaraza zaidi ya 700,walichokileta ni tafsiri yao kuhusu maoni hayo, mnielewe vizuri hapo na wao walikaa tume wakachambua mengine waliyakataa mengine wakayaacha mengine wakarekebisha,” alisema na kuongeza;

 

“Ingekuwa ni kuleta yote maoni ya wananchi ingekuwa ni book (kitabu) ambalo hatuwezi hata kulibeba lakini Tume ilifanya kazi yake, lakini kama ilivyo kazi yoyote ya binadamu ina kasoro za hapa na pale,chombo cha juu cha Tume ni Bunge hili… lina wajibu wake lenyewe halitarajiwi kutoa rasimu bali litatoa katiba inayopendekezwa ndio maana katika kipindi hiki tumeendelea na makundi mbalimbali na ninyi wenyewe mmeona yamekuwa msaada mkubwa yametoa maoni na mengine yamekubalika ili kuboresha katiba.”

 

Aliongeza kuwa lengo na madhumuni ya wajumbe wa Bunge hilo ni pamoja na katiba watakayoitunga iwe katiba ambayo itawezesha sheria zitakazokuwa rafiki kwa Watanzania wote hususan wanyonge,wakulima wa kawaida na wafanyabiashara wadogo.

 

Hata hivyo, aliwataka wajumbe wa Bunge hilo kutofadhaika na maneno ya kejeli wanayotupiwa hasa kuhusu posho na mambo mengine kwani yeye kama mwenyekiti wa Bunge hilo yupo imara.

 

“Mimi mwenyekiti wenu nipo imara na kwa hulka yangu mimi hizi kejeli, matusi ni kama vile maji katika mgongo wa bata haloani kwa hiyo waendelee tu pengine tunaanza kuwabaini,” alisema na kusisitiza;

 

“Kuna rafiki yangu mmoja anaitwa Kubenea (Said),jamani karne za nyuma ya 15,16,17 wafalme wa kule Ulaya walikuwa na watu… wafalme wa Ulaya waliajiri wachekeshaji kwa malengo mawili moja ni kumsikia mfalme kwa kila kitu, nyingine ni kuwasema wote ambao mfalme ni wabaya wake kwa hiyo kuna watu wa namna hii tunaanza kuwaona sasa kama Kubenea ni mchekeshaji wa mfalme… yeye kuna mfadhili na wafadhili nyuma yake wanamsogeza mbele kwa sababu wanaona vipaji vyake vya kukubali kufanya kazi kama hizo; kwa hiyo tuwaone nao kuna njia nyingi za kupata riziki tuwasemehe tu waendelee na shughuli zao,” alisema.

 

Awali, alitoa utaratibu wa shughuli za bunge hilo hasa jinsi ya kuwasilisha taarifa za kamati 12. Alisema baada ya mwenyekiti kuwasilisha taarifa ya kamati yake kwa sura zote kamati ya uongozi imepanga kila siku katika ya siku tano za kupokea taarifa wenyeviti wote watapitia sura zilizoteuliwa ambapo kwa jana walipitia sura namba 2,3,4 na 5.

 

Sitta alisema sababu ya kufanya hivyo ni pamoja na kuwa na uangalifu wa sura chache chache kuliko kamati moja kumaliza sura zote kwani kwa kufanya hivyo itakuwa na mambo mengi.

Aliongeza kuwa maoni ya wengi yatasomwa kwa dakika 20 huku ya wachache yakisomwa kwa dakika 10.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 maoni:

Post a Comment