Klabu ya Azam FC leo itakuwa na shughuli pevu kusaka nusu fainali ya michuano ya Kombe la Mapinduzi pale itakapochuana na Jamhuri Uwanja wa Amaan, Zanzibar saa 2.15 usiku.
Azam wakiingia dimbani kupambana na Zimamoto

Azam FC ilianza vema michuano hiyo jana kwa kuichapa Zimamoto, bao likifungwa na Shaaban Idd dakika ya 79 akiunganisha krosi safi iliyochongwa na Salum Abubakar ‘Sure Boy’.
Jamhuri ambayo iliambulia kipigo kizito cha mabao 6-0 juzi dhidi ya Yanga, nayo itakuwa ikisaka ushindi ili kurejesha matumaini ya kusonga mbele.

Kocha Mkuu wa muda wa Azam FC, Idd Nassor Cheche, ameweka wazi kuwa wanauchukulia kwa uzito mchezo huo huku akiongeza kuwa amerekebisha udhaifu ulijitokeza kwenye mchezo wa awali.
“Wachezaji wangu waliidharau timu pinzani kwenye mchezo wa awali, pia safu ya ushambuliaji ilicheza kwa kuridhika, tayari mechi ya kwanza imewapa somo kwa hiyo nafikiri mechi inayofuatia watafanya vizuri zaidi na kupata matokeo bora,” amesema.

Mechi nyingine leo itakuwa ni kati ya Zimamoto na Yanga mchezo utakaopigwa saa 10:00 jioni.
Hadi hivi sasa kuelekea mechi za pili za Kundi B la michuano hiyo, Yanga ndio ipo kileleni ikiwa na pointi tatu sawa na Azam FC lakini inaizidi kwa mabao ya kufunga (tofauti ya mabao matano).
Tofauti hiyo inatokana na Yanga kushinda mabao 6-0 kwenye mchezo wa awali dhidi ya Jamhuri huku Azam FC ikiibuka na ushindi wa 1-0 walipotangulia kucheza na Zimamoto.

Timu za Zimamoto na Jamhuri zote kutoka Zanzibar zilizopoteza mechi zao za awali, zinafuatia kwenye msimamo huo katika nafasi ya tatu na nne zikiwa hazina pointi hata moja